RAISI KIKWETE APOKEA BARUA YA MAZUNGUMZO JUU YA SHERIA YA KATIBA MPYA KUTOKA KWA VIONGOZI WA CHADEMA - LUKAZA BLOG

All You Want is Here | Chochote Unachohitaji Utakipata Hapa

Habari Mpya

RAISI KIKWETE APOKEA BARUA YA MAZUNGUMZO JUU YA SHERIA YA KATIBA MPYA KUTOKA KWA VIONGOZI WA CHADEMA

Taarifa ya TBC imeeleza kuwa Rais Jakaya Kikwete amepokea kwa furaha ombi la viongozi wa CHADEMA la kutaka kuonana naye ili kuzungumzia sheria ya mchakato wa uandaaji wa katiba, na amewaagiza maafisa wake kuandaa mkutano huo. Kwangu mimi naona hii ni busara kubwa ambayo Rais ameonesha tofauti na baadhi ya watu ambao wangependa Rais akatae. Wapo pia wale ambao hawakupenda viongozi wa CHADEMA kutoa ombi hilo kwa Rais, wangependa mara moja maandamano yaanze bila ya nafasi yoyote ya kufanya mazungumzo. Kwangu mimi, kama dhamira yetu ni kupata katiba iliyo nzuri, na hakuna hila upande wowote nyuma yake, tuna haki ya kumpongeza Rais JK na viongozi wa CHADEMA kwa kuruhusu mazungumzo kwanza kabla ya jitihada nyingine zozote.
 
Ombi langu kwa Rais na kwa viongozi wa CHADEMA waende katika mjadala huo kwa dhamira moja kubwa - YA KUPATA KATIBA ILIYO BORA. Dhamira ya viongozi wa CHADEMA na RAIS iwe ni kupata katiba iliyo bora kabisa Afrika, kwa sababu hilo linawezekana kama tukinuia. Kusiwe na mawazo ya kutafuta ushindi, na kila upande uwe tayari kuusikiliza upande mwingine, kila upande ukiamini kuwa wote wana dhamira njema. 
 
Siyo mjadala wa mashindano kati ya Rais na CHADEMA au CCM na CHADEMA, uwe ni mjadala wa kupata katiba iliyo bora kabisa katika Taifa letu. Nawashauri Jukwaa la Katiba, nao wachukue kwanza njia hii ambayo CHADEMA wameamua kuichukua kuliko kwenda kwenye maandamano bila ya kuwa na uhakika kuwa matakwa yao Rais anaweza kuyasikiliza au la. Tufahamu kuwa bado haijawa sheria, itakuwa sheria tu baada ya Rais JK kuweka saini yake. Rais toka Mwanzo amechukua msimamo tofauti kuhusu suala la katiba. 
 
Tukumbuke kuwa Waziri wa sheria alikataa, mwanasheria mkuu alikataa, na wengi ndani ya CCM walitamka hakuwezi kuwa na katiba mpya. Rais JK akatamka wazi kuwa Tanzania itapata katiba mpya. Nina imani Rais kama binadamu yeyote, baada ya baadhi ya viongozi wenzie kusema hakuna haja ya kuwa na katiba mpya, na yeye kutofautiana nao, hatakuwa tayari kuwapa nafasi wale waliokuwa wakipinga waonekane kuwa walikuwa sahihi. Nadhani Rais atapenda jambo hili lifanikiwe. 
 
Kwa JK hii ndiyo itakuwa 'legacy' yake kubwa katika Taifa hili, itakayodumu kwa miaka mingi. Namshauri Rais, katika hili la katiba ashirikiane na mtu yeyote mwenye nia njema ya kupata katiba nzuri bila ya kujali mtu huyo ana itikadi gani. Na wale wote tunaolalamikia katiba iliyopo, na sheria iliyopitishwa hivi karibuni ili kupata katiba mpya, kwa kuwa inaonekana Rais yupo tayari kutoa nafasi kwa yeyote ya kusikilizwa, tuitumie nafasi hii vizuri, tukijadiliana na kushauriana kwa dhamira njema.
 
  Tundu Lisu, ni mwanabidii, na yupo kwenye ile kamati ya kwenda kuonana na Rais, tunawaombeni mkaitumie nafasi hii vizuri, dhamira ikiwa ni kupata katiba bora na wala siyo kutafuta mshindi kati ya CHADEMA na Rais au CHADEMA na CCM. Tunawaombeeni wote, ili muongozwe na hekima katika mjadala wenu maana inawezekana kabisa kupata katiba nzuri kwa amani na maelewano. HONGERA RAIS, HONGERA CHADEMA KWA KUFUATA NJIA YA MAZUNGUMZO. Taifa letu na watu wake ni muhimu kuliko mtu yeyote, kuliko chama chochote.

No comments:

Post a Comment

Tafadhari Maoni Yenye Matusi Hayatakuwa Publish Tutoe Maoni Bila Kuumiza Wala Kujeruhi Hisia Za Mtu.....@(Sponsored By Lukaza Blog)


Pages