NENO LA LEO: S'TOKI JIKONI, TUI LANGU SIJE FURUMIA - LUKAZA BLOG

All You Want is Here | Chochote Unachohitaji Utakipata Hapa

Habari Mpya

NENO LA LEO: S'TOKI JIKONI, TUI LANGU SIJE FURUMIA

 
Ndugu Zangu,
Niliwaahidi kuwaletea tafsiri yangu ya kilichotokea Gongo La Mboto. Nilishindwa juzi ile kwa vile nilikuwa na tui jikoni. Jamani, tui halijakatika, linachemka kweli na chumvi n'shatia. Na kesho ndo kesho, asiye mwana aeleke jiwe. Mchele n'loloweka ndo n'tautia tuini. Kwenye tui lichemkalo.


Hata kama niko jikoni, lakini mwenzenu nayasikia ya nje ya jiko; mathalan, habari, kuwa Ghadafi maji yamemfika shingoni. Naye kazidi, mwanzo wa mwisho wake umeshaingia.

Halafu tena, si nimesikia, kuwa ' Sheikh wa Dowans' kaingia mjini. Na kwenye mitambo yake kule Ubungo katembelea! Ama, makubwa ati! Si mmiliki alikuwa hajulikani?

Leo Sheikh wa Dowans, huku akiwa amevalia kanzu, baraghashea na malapa miguuni kaonekana Ubungo. Na kesho si ni Ijumaa.

Hivi kuna ajuaye Sheikh wa Dowans ataswali wapi Ijumaa; Msikiti wa Mtoro, Tambaza au Mtambani? Ingekuwa vema, baadhi ya wazee wenye hikma wa jiji wakazungumze nae mara baada ya swala ya Ijumaa.

Wamsimulie kisa cha Abu- Dowans, samahani Abunuwas. Naam. Abunuwas alipata kumnunua punda sokoni. Akapita nae kwa jirani yake hadi akaingia nae nyumbani kwake. Jirani yake alipomwona Abunuwas na Punda akaenda kwa Abunuwas kutaka kuazima punda.

Jirani; " Abunuwas, naomba uniazime punda wako nikabebee mzigo wangu"

Abunuwas; :" E bwana we, mie sina punda"

Mara punda akasikika uani akitoa mlio. Jirani akatamka; " E rafiki yangu Abunuwas, mbona nausikia mlio wa punda!"

Abunuwas; " E bwana we, nimekwambia sina punda, lakini, kama wataka kuazima mlio chukua!"

Naam. Sheikh wa Dowans aambiwe, kuwa Watanzania hatulipi deni lake! Si tuliambiwa, kuwa Richmond ilikuwa kampuni hewa! Inakuwaje basi, ' Abu- Dowans' anunue mitambo ya kampuni hewa? Kwa mantiki hiyo, tutashindwaje kuamini, kuwa deni la bilioni 94 la Sheikh wa Dowans, bwana Abu- Dowans ni deni hewa. Hapa kuna wanaofanya biashara na uchumi wetu.

Na kama si hofu ya tui langu kufurumia, hakika ningeendelea kusema, we acha tu....
Nimeshasema; S'toki Jikoni, Tui Langu Sije Furumia! Na hilo ni Neno La Leo.

Maggid

Dar es Salaam.
Februari 24, 2011
http://mjengwa.blogspot.com

No comments:

Post a Comment

Tafadhari Maoni Yenye Matusi Hayatakuwa Publish Tutoe Maoni Bila Kuumiza Wala Kujeruhi Hisia Za Mtu.....@(Sponsored By Lukaza Blog)


Pages