Maandalizi maziko ya Mgimwa ukingoni - LUKAZA BLOG

All You Want is Here | Chochote Unachohitaji Utakipata Hapa

Habari Mpya

Maandalizi maziko ya Mgimwa ukingoni

MAANDALIZI ya maziko ya aliyekuwa Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa, yameendelea katika hatua za mwisho, ambapo jana Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliwasili mjini Iringa asubuhi kukagua maandalizi hayo. Baada ya kuwasili, Pinda alikwenda moja kwa moja katika Kijiji cha Magunga Tarafa ya Kiponzelo wilayani Iringa, kukagua maandalizi ya maziko hayo yatakayofanyika leo, nyumbani kwake katika makaburi ya familia kilometa 66 kutoka Iringa mjini.

Alipowasili katika Uwanja wa Ndege wa Nduli na kupokewa na viongozi wa Mkoa wa CCM na Serikali na kufika nyumbani hapo, Pinda aliwapa pole mama mzazi wa Dk Mgimwa, Consolata Semgovano, wajomba zake na wafiwa wengine. Pia alikagua ujenzi wa kaburi atakamozikwa leo, uwekaji wa mahema, eneo la kufanyia ibada ya maziko na mahali mwili wa marehemu utakapolazwa.

Alipomaliza ukaguzi, Waziri Mkuu alirejea mjini Iringa kuusubiri mwili wa Dk Mgimwa ambao ulitarajiwa kuwasili Uwanja wa Ndege wa Nduli jana jioni na kwenda kuagwa na wakazi wa Iringa kwenye ukumbi wa ‘Siasa ni Kilimo’ na baadaye kupelekwa Magunga ambako utalala nyumbani kwake.
Dar es Salaam wamuaga Wakati huo huo, jana mamia ya wakazi wa Dar es Salaam, viongozi wa Serikali, wabunge, mabalozi wa nchi mbalimbali wakiongozwa na Rais Jakaya Kikwete, jana walijitokeza kuuaga mwili wa Dk Mgimwa katika Viwanja vya Karimjee.

Dk Mgimwa alizaliwa mwaka 1950 Magunga na kufariki Januari mosi  katika Hospitali ya Kloof Medi-Clinic nchini Afrika Kusini baada ya kusumbuliwa na ugonjwa wa figo. Miongoni mwa waliojitokeza kumuaga mbali na Rais Kikwete ni Makamu wa Rais, Dk Mohamed Ghalib Bilal, mjane wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Mama Maria na Spika wa Bunge Anne Makinda.

Wengine ni mke wa Rais, Mama Salma Kikwete, makatibu wakuu wa wizara mbalimbali na manaibu wao, viongozi wa vyama vya siasa pamoja na Waziri wa Fedha wa Uganda, Aston Kajala aliyewakilisha mawaziri wa fedha kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Akizungumzia utendaji wa Dk Mgimwa, Spika Makinda alisema alikuwa kielelezo kikubwa cha uongozi ndani ya Bunge na Serikali kwa utendaji wake wa kujituma bila kuchoka huku akifanikisha kikamilifu mabadiliko ya mfumo wa bajeti.

Alisema kifo cha Dk Mgimwa ni mtihani mzito kwa Rais, hasa katika kumpata kiongozi mwingine atakayefaa ‘kuvaa viatu vyake’ katika Wizara hiyo nyeti hapa nchini huku akisisitiza kuendelezwa kwa mbegu bora zilizopandwa na kiongozi huyo enzi za uhai wake. “Wallah kama tungekuwa tunaambiwa tubadilishe mtu wa kwenda huko, Mgimwa tungesema abaki tungechagua mtu mwingine wa kwenda lakini kwa sababu ni mapenzi ya Mungu aende na akapumzike kwa amani,” alirudia usemi wake Makinda.

Naibu Waziri wa Wizara ya Fedha, Saada Mkuya alimsifu Dk Mgimwa kwa uchapakazi na ushirikiano aliokuwa nao kwa wafanyakazi wote wa wizara hiyo. Alisema bila kujali nafasi ya kila mmoja ndani ya wizara hiyo, Dk Mgimwa alijali na kusikiliza mawazo ya kila mtu.

Kwao alikuwa mtumishi shupavu aliyeamini katika nguvu za hoja na mawazo ya kila mtu huku akisisitiza kuwa ingawa pengo lake ni gumu kuzibika, lakini watafanya kazi kwa kufuata matendo mema waliyojifunza kupitia kwake. Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alisema Dk Mgimwa ni kiongozi aliyekuwa na ushirikiano kwa wabunge wote bila kujali itikadi za vyama wanavyotokea, jambo alilosema halionekani kwa viongozi wengine.


Katibu wa Wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Jenister Muhagama alisema Dk Mgimwa ameacha pengo lisilozibika ndani ya Serikali na chama kutokana na umakini na busara aliyokuwa nayo wakati wote wa uongozi na uhai wake. Chanzo Habari Leo

No comments:

Post a Comment

Tafadhari Maoni Yenye Matusi Hayatakuwa Publish Tutoe Maoni Bila Kuumiza Wala Kujeruhi Hisia Za Mtu.....@(Sponsored By Lukaza Blog)


Pages