Wanafunzi 15 Chuo Kikuu St John wasimamishwa - LUKAZA BLOG

All You Want is Here | Chochote Unachohitaji Utakipata Hapa

Habari Mpya

Wanafunzi 15 Chuo Kikuu St John wasimamishwa

WANAFUNZI 15 wa Shahada ya Kwanza ya Elimu na Sanaa katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu
John, mkoani Dodoma wamesimamishwa masomo huku waliobaki wakipewa masharti ya kurudi chuoni hapo.

Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Ofisa Uhusiano wa chuo hicho, Karim Meshack imesema kati ya hao waliosimamishwa hadi taarifa nyingine itakapotolewa, 13 ni wa mwaka wa pili na mmoja ni wa mwaka wa tatu.


Wanafunzi hao wametajwa kuwa ni Albert Mganga, Ayub Benjamini, Erick Mkunda, Frank 
Nicodemo, Goodluck Gadway, John Komba na Kapinga Wilson.

Wengine ni Leba Camus, Masatu Siajali, Mbogo Lyoba, Milawi Stephen, Mohamed Shambi, 
Mwaipasi Brown, Mwinyi Ally na Pasquina Ferdenand.

Masharti hayo ni pamoja na kila mwanafunzi kutakiwa kujisajili ndani ya siku mbili na kama 
atashindwa kufanya hivyo basi atakuwa amejifukuza mwenyewe na madarasa yanatarajiwa kuanza Januari 4 mwakani.

Taarifa hiyo ilisema kuwa, wanafunzi hao wanatakiwa kulipa ada ya chuo ifikapo Desemba 29.


Wanatakiwa kuonesha risiti za malipo za benki ambayo itakuwa na jina la mwanafunzi na namba yake ya usajili.


Kwa mujibu wa taarifa hiyo pia kila mwanafunzi anatakiwa kujaza fomu za makubaliano ambazo zinapatikana katika mtandao wa chuo.


Pia hakuna mwanafunzi atakayeruhusiwa kuingia chuoni hapo bila kusajiliwa.Usajili huo
utafanyika jengo la utawala.

“Katika kipindi cha wiki mbili kuanzia Januari 2 hadi Januari 15 mwakani wanafunzi wote
wanatakiwa kuwa na hati za usajili na kutakuwa na ukaguzi unaofanywa mara kwa mara kuangalia kama wanafunzi hao wamejisajili,” ilisema taarifa hiyo.

Taarifa hiyo ilisema kuwa, fedha kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kwa ajili ya wanafunzi 2,400 wanaostahili kupata fedha hizo, zimefika na zimeanza kuingizwa kwa wanafunzi ambao wamekamilisha taratibu zote za usajili.


Desemba 21 mwaka huu, baadhi ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha St John kampasi ya Mazengo walifanya mgomo wa kushinikiza kupewa robo ya pili ya fedha za kujikimu kutoka Heslb.
 Imeandikwa na Sifa Lubasi, Dodoma wa Habari Leo

No comments:

Post a Comment

Tafadhari Maoni Yenye Matusi Hayatakuwa Publish Tutoe Maoni Bila Kuumiza Wala Kujeruhi Hisia Za Mtu.....@(Sponsored By Lukaza Blog)


Pages