Kikwete tambua kuwa Watanzania hatuwezi kufunga jalada la Richmond Kirahisi hivi - LUKAZA BLOG

All You Want is Here | Chochote Unachohitaji Utakipata Hapa

Habari Mpya

Kikwete tambua kuwa Watanzania hatuwezi kufunga jalada la Richmond Kirahisi hivi

https://mail.google.com/mail/?ui=2&ik=3530edf2ab&view=att&th=1340e401ad6e498a&attid=0.1&disp=inline&realattid=f_gvtgyqg10&zw 
Na Nova Kambota Mwanaharakati,

Nianze makala yangu kwa kutamka wazi kuwa sikubaliani na kauli mbiu ya miaka hamsini ya uhuru wa Tanzania bara ‘’tumeweza, tumethubutu, tunasonga mbele’’ sikubaliani na dhana hii na kamwe sitakubaliana nayo kwasababu kila Mtanzania anayejua ukweli tena ni mzalendo anatambua wazi jinsi taifa letu linavyorudi nyuma kwa kasi ya ajabu ndani ya miaka hii hamsini, sasa watu wanahoji tumethubutu nini? Kama sio porojo hizi?

Baada ya utangulizi huo sasa nije kwenye hili nalotaka kulizungumzia leo, hili ni maalumu kwa rais wa jamuhuri ya muungano wa Tanzania Mh Jakaya Kikwete , sina uhakika ni mara ngapi huwa anasoma makala zangu lakini nachoamini kuwa kila anapopata nafasi hiyo huwa anapitia maandiko yangu hivyo naandika makala hii nikiwa na imani kuwa ataisoma kama si yeye basi wapambe wake wataipitia.

Baada ya kumalizika kwa kikao cha CCM huko Dodoma naona watanzania wamerejea katika majukumu yao ya kila siku na maisha yanataka kulazimishwa kuendelea kama kawaida huku akili za kawaida zikitushawishi pasi na shaka kuwa hali haipo kawaida hasa kwa upande wa rais wetu Kikwete  kutokana nayeye kutajwa kwenye kashfa ya Richmond.

Nisingependa kurudia kile ambacho tayari kimeshazungumzwa na waandishi wengine juu ya alichofanya Lowassa kwa kumtaja waziwazi rais Kikwete na uhusika wake ndani ya kashfa hiyo ya kampuni hewa ya ufuaji umeme ya Richmond ambayo hakuna ubishi kuwa itachukua karne nyingi mpaka mzimu wa kampuni hii ufutike kabisa kwenye akili za watanzania.

Tuhuma dhidi ya Kikwete zimekuwepo kwa muda mrefu lakini tofauti na sasa ambapo alichofanya Lowassa si tu kumtuhumu Kikwete bali kumtaka akumbuke kile ambacho kinaweza kutafsiriwa ni ‘’UCHAFU WAKE’’. Tuhuma za Lowassa zimesemwa ndani ya kikao cha CCM tena mbele ya Kikwete mwenyewe ambaye angeweza kuzijibu au la, lakini kwa hiyari  yake amekaa kimya, je hii inatafsiri gani? Lowassa amesema ukweli? Kikwete anamwogopa Lowassa? au tusubiri vita kati ya maswahiba hawa wawili? ambao kadri muda unavyoenda dalili zinaonyesha watazidi kuraruana na mwishowe watatangaza kuwa ‘’WALIKUTANA TU BARARANI’’ tofauti na awali ambapo walijifanya ni marafiki wa kweli.

Juhudi zozote za CCM, Ikulu au Kikwete mwenyewe kutosema wazi ushiriki  wa Kikwete katika sakata hilo haziwezi kutufanya watanzania tuamini kuwa ‘’Kikwete hahusiki’’ huku tunajua wazi ni kwa kiasi gani Lowassa anamfahamu Kikwete kwa undani?. Wimbo ni huu kama kuna ‘’mpuuzi’’ anayedhani jalada la Richmond limefungwa basi ajue anajidanganya, sisi watanzania hatuwezi kukubali kumaliza mjadala mpaka pale uchunguzi wa kina utakapofanyika dhidi ya mtuhumiwa mpya kwenye sakata hilo ambaye ni rais Kikwete. Naam! Kikwete yakupasa utambue kuwa watanzania hatuwezi kukubali sakata la Richmond liishe kirahisi hivi , tunataka ‘’UCHUNGUZI HURU NA WAHAKI.
 
A luta Continua!
 
Nova Kambota,
+255717 709618
novakambota@gmail.com
www.novakambota.com
Tanzania, East Africa
Monday 5, December 2011.

No comments:

Post a Comment

Tafadhari Maoni Yenye Matusi Hayatakuwa Publish Tutoe Maoni Bila Kuumiza Wala Kujeruhi Hisia Za Mtu.....@(Sponsored By Lukaza Blog)


Pages