Wananchi wa mji mdogo wa Mbalizi, wilaya ya Mbeya Vijijini
mkoani Mbeya wakigombania foleni ya kuteka maji, yaliyobebwa kwenye
Behewa la treni inayomilikiwa na Shirika la Reli la Tanzania na Zambia
(TAZARA) siku ya jana majira ya asubuhi kutokana na uhaba wa maji
unaokabiri mji huo.
Wananchi waliofika eneo TAZARA huku wengine wakiwa wamepanga
foleni kwa ajili ya kupata maji ambapo Shirika la Reli la Tanzania na Zambia (TAZARA) liliteka maji hayo kwa ajili ya wafanyakazi wake
waliopo mji mdogo wa Mbalizi, wilaya ya Mbeya vijijini Mkoani Mbeya.
Wananchi
waliofika eneo TAZARA huku wengine wakiwa wamepanga foleni kwa ajili
ya kupata maji ambapo Shirika la Reli
la Tanzania na Zambia (TAZARA) liliteka
maji hayo kwa ajili ya wafanyakazi wake waliopo mji mdogo wa Mbalizi,
wilaya ya Mbeya vijijini Mkoani Mbeya.
*****
Siku ya tatu toka hali ya utulivu
kurejea mkoani Mbeya, hali imekuwa tete zaidi katika mji mdogo wa
Mbalizi uliopo wilaya ya Mbeya Vijijini ambapo wananchi wanamtaka Mkuu
wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro kuchukua maamuzi mazito ya
kuwarejeshea mradi wao wa maji ulioporwa na Vigogo wa Serikali.
Vikosi kadhaa vya kutuliza Ghasia (FFU)
vilionekana jana katika viunga mbalimbali vya mji huo kwa ajili ya
kuwatawanya wananchi baada ya Serikali kupata taarifa yakuwepo
maandalizi ya maandamano ya kudai haki yao hiyo ambayo walisema Mkuu
wa wilaya hiyo Evance Balama alishindwa kuitolea ufafanuzi katika
mkutano uliofanyika Kijijini hapo hivi karibuni.
Wakizungumza na waandishi wa habari mjini
Mbalizi leo, wananchi ambao waliomba hifadhi ya majina yao walisema
kuwa wanamuomba Mkuu wa mkoa wa Mbeya kuingilia kati shida ya maji
inayoukabili mji huo ili kuwanusuru na hali mbaya ya ukosefu wa maji
ambayo kwa sasa hununua lita 20 kwa Shilingi 1500 maji ambayo yanatoka
Jijini Mbeya.
Wakati FFU wakiwa wanazunguka katika mji huo
kuhakikisha hazitokei vurugu, wananchi kadhaa walionekana
wakigombania matone ya maji yaliyokuwa yamepelekwa eneo la Tazara na
Shirika la Tanzania na Zambia.
Kwa mujibu wa
baadhi ya maafisa wa Tazara ambao walihojiwa na mtandao huu wamesema
kuwa maji hayo ambayo yalikuwa ndani ya behewa moja la gari
moshi(Treni) yalikuwa maalum kwa ajili ya familia za wafanyakazi wa
Tazara wanaoishi katika Mji huo lakini wananchi baada ya kuona hivyo
wakajikusanya na kuanza kuchota maji hayo.
Hali hiyo ilianza
majira ya saa kumi jioni Novemba 13 mpaka jana majira ya saa Nne
asubuhi ambapo maji yalikuwa yamekwisha lakini imeelezwa kuwa baada ya
kuona hivyo Serikali imeamua kuwaangukia Tazara ili waendelee
kuwapelekea maji wananchi hao ili kuinusuru Serikali kuingia katika
vurugu na wananchi hao.
Novemba 9, mwaka
huu wananchi hao walimtaka Rais Jakaya Kikwete kumfuta kazi haraka ama
kumwondoa wilayani humo Mkurugenzi wa wilaya hiyo, Juliana Malange
kutokana na kushindwa kudhibiti genge la waporaji wa miradi ya
wananchi.
Hayo waliyasema
katika mkutano wa hadhara uliokuwa umeitishwa na Mkuu wa wilaya hiyo
Evance Balama kwa nia ya kutatua kero ya maji ambayo wanatozwa kwa
amri Shilingi Elfu kumi na Mamlaka ya maji iliyopelekwa kinyemela na
Serikali kijijini hapo huku kikao hicho kikishindwa kutoa majibu kwa
wananchi.
Wananchi hao
walimweleza Mkuu huyo wa wilaya kuwa tatizo hilo limesababishwa na
Mkurugenzi huyo ambaye amekiweka Kijiji hicho kama shamba la Bibi la
kuchumia fedha bila kushirikiana na wananchi huku akitumia wapambe wake
kupora miradi ya wananchi na kujimilikisha ukiwemo mradi huo.
Baadhi ya mabango
hayo yaliandikwa ‘’Tumechoka na bili hewa, ,Hivi maji ni ya Minja na
Mkurugenzi, Minja + Gadafi= na uuaji, Wazee wetu walichimba mitaro,
Minja tupe maji yetu’’
Wananchi hao zaidi ya Elfu ishirini
waliokusanyika katika viwanja vya mahubiri kutoa kero zao walimuuliza
Mkuu huyo maswali zaidi ya ishirini ambayo yote hayakupatiwa majibu
badala yake Mkuu huyo wa wilaya aliomba radhi kwa yale yote
waliyotendewa wananchi kabla na baada ya kuhamishiwa yeye katika
wilaya hiyo.
Naye Elia
Kabholile alisema kuwa alishangaa kuona Mkurugenzi ameambatana na Mkuu
wa wilaya wakati alikuwa ameitwa na wananchi akawapuuza kutokanana
hulka yake ya kuwa na kiburi.
Baada ya hapo
Mkuu wa wilaya alimwita Mkurugenzi wake Juliana Malange ili ajibu yale
yanayomuhusu na shutuma alizokuwa akitupiwa ana kwa ana na wananchi
hali iliyozua mtafaruku baada ya Mkurugenzi huyo kukataa kujibu
shutuma zake akiwa juu ya jukwaa la meza.
Kutokana na hali
hiyo huku wananchi wakimtaka apande katika meza iliyokuwa ikitumiwa na
viongozi wenzake kujibu hoja na kuhoji ndipo akaanza kubembelezwa na
viongozi wenzake huku akizomewa na wananchi wakisema kuwa amekuwa
shalobalo hivyo aondoke.
Hali hiyo ilileta
mzozo mkubwa, huku Mkuu wa wilaya hiyo akiamua kuchukua makarabrasha
yake na kuondoka bila mkutano kufungwa huku wananchi wakiendelea
kumzomea Mkurugenzi na kutaka kumpiga mawe Meneja wa maji Andason
Minja waliyemwita ‘’Ninja’’ aliyekuwa amefishwa katika gari STK 7534
huku msafara huo ukiokolewa na Polisi waliokuwa wakiongozwa na Kamanda
wa polisi wa wilaya hiyo Silvester Ibrahim.
Kutokana na ubabe
huo wa baadhi ya watendaji wa Serikali ya wilaya hiyo kupora mradi wa
maji, hivi karibuni wananchi wa Kijiji hicho walifunga ofisi za
mamlaka hiyo ambayo mpaka sasa haijafunguliwa mpaka hapo mradi
utakaporejeshwa mikononi mwa Serikali ya Kijiji.Habari Na Mbeya Yetu Blogu
No comments:
Post a Comment
Tafadhari Maoni Yenye Matusi Hayatakuwa Publish Tutoe Maoni Bila Kuumiza Wala Kujeruhi Hisia Za Mtu.....@(Sponsored By Lukaza Blog)