Mtoto anapotafuta mzazi bandia kuficha uovu shuleni - LUKAZA BLOG

All You Want is Here | Chochote Unachohitaji Utakipata Hapa

Habari Mpya

Mtoto anapotafuta mzazi bandia kuficha uovu shuleni

http://habarileo.co.tz/images/ikonko.jpg
Imeandikwa Na Nicodemus Ikonko

WAZAZI wa kizazi chetu hiki tuna changamoto lukuki katika suala zima la malezi ya watoto wetu. Moja kati ya changamoto tunazokabiliana nazo na ambazo kwa bahati mbaya hatuwezi kuzikwepa ni pamoja na malezi ya watoto wetu.





Tunapoamka asubuhi kila mzazi makini tayari huanza mapema kabisa kukimbizana na ratiba yake ya siku hiyo. Kuna wanaokwenda mashambani, maofisini, viwandani ama kwenye biashara zao. Inapofika jioni wengine bado huwa kwenye pilikapika na wengine wakienda madarasani ili kujiongezea ujuzi.
Lakini kwa upande wa pili wa shilingi wazazi tunalo jukumu kubwa la kuwalea watoto wetu kwa maana ya kusimamia elimu zao, afya zao, mavazi yao na mahusiano yao mema na jamii.

Majukumu hayo hatuna namna ya kuyakwepa. Changamoto hizi sasa zinapata ukali zaidi kutokana na mfumo wa maisha unaosongwa na utandawazi kwa maana ya kurahisishwa kwa mfumo wa mawasiliano ya simu za mkononi, mtandao wa kompyuta, mitandao ya kijamii kama vile Facebook, twitter, YouTube na mingine mingi.

Utandawazi kwa ujumla unawapatia maarifa na ujanja watoto wetu, yakiwemo mazuri kama mtoto atajielekeza huko lakini kuna maarifa mabaya pia atakayopata kama wazazi wakijisahau na haya mabaya ni haraka sana kwa watoto kuyakimbilia.

Kama Mzazi, safu yako hii leo ingependa ikumegee kisa kimoja kilichotokea hivi karibuni jijini Dar es Salaam katika moja ya sekondari zetu za kata. Kutokana na maadili ya kazi hii, nisingependa kuitaja shule husika. Mzazi mmoja anayejali malezi ya watoto wetu ndiye aliyenisimulia kisa hiki tulipokutana baada ya kazi za kutwa nzima.

Alisema mwanafunzi mmoja wa shule ya sekondari ya kata alifanya kosa kubwa shuleni lakini walimu hawakupenda kumpatia adhabu moja kwa moja hadi aende na mzazi wake. Kutokana na uzito wa kosa lenyewe hakuruhusiwa kuingia darasani. Kwa bahati nzuri mwanafunzi husika alijua jinsi wazazi wake walivyo makini na ambavyo hawataki mchezo kwa masuala yanayohusu nidhamu ya watoto.

Kijana haraka haraka akapanga jinsi ya kupotezea au kutatua suala hilo bila wazazi wake kujua. Kwa mujibu wa mzazi aliyenipa kisa hiki, kijana akazua ishu kwa wazazi wake wampatie fedha kiasi kadhaa kwa madai kwamba zinahitajika kwa ajili ya masuala ya kwenda ziara ya kimasomo na wazazi bila hiana wakampatia fedha hizo.

Akazichukua na kumtafuta njemba mmoja na kumweleza yanayomsibu na kumtaka aende naye shuleni kwake akazungumze na walimu kwa kujifanya ndiye mzazi wake halisi. Akamkatia 'pochi' na bila kusita jamaa akaongozana naye hadi shule kama walivyokubaliana. Lakini alipofika na kuonana na walimu na kuelezwa kinagaubaga kosa la mwanafunzi huyo, 'mzazi' huyo alimgeuka palepale na kuanza kumwadhibu kwa fimbo mbele ya walimu wake. Ghafla kijana naye akavimba.

Akaanza kumrushia ngumu ‘mzazi wake’ huku maneno yakimtoka kwamba alimlipa ili amtetee na siyo kumwadhibu na kumwumbua mbele ya walimu wake. Siri ikafichuka na ndipo walimu walipobaini kuwa kumbe walikuwa na mzazi bandia na hivyo kumlazimisha kijana akawalete wazazi wake halisi. Mpo hapo wazazi wenzangu?

Tuimarishe mawasiliano baina ya walimu, wazazi au walezi na wanafunzi ili sote kwa pamoja tuzungumze lugha moja badala ya kusubiri kuchezewa mchezo wa kuigiza kama huu.

Usikose safi hii Jumatatu ijayo. O766 843382 nvikonko@gmail.com

Chanzo: Mwananchi Online.

No comments:

Post a Comment

Tafadhari Maoni Yenye Matusi Hayatakuwa Publish Tutoe Maoni Bila Kuumiza Wala Kujeruhi Hisia Za Mtu.....@(Sponsored By Lukaza Blog)


Pages