ABIRIA
aliyefahamika kwa jina moja la Amina mkazi wa wilaya ya Mbozi mkoani
Mbeya alikufa papo hapo katika ajali iliyotokea juzi usiku katika Kituo
cha Mabasi yaendayo Mikoani kutokea Mbeya baada ya basi la New Force
kuparamia ukuta wa mgahawa uliopo mkabala na Ofisi za Mabasi ya Kampuni
hilo.
Tukio hilo limetokea majira ya
saa 5:00 usiku wa Ijumaa ya Januari 20 mwaka huu katika Kituo hicho cha
Mabasi yakitokea mikoa mingine.
Mashuhuda
wa tukio hilo wamesema kondakta wa basi hilo aliyejulikana kwa jina la
Januari Kapinga aliingia ndani ya basi hilo lenye namba za usajili T 853
AVQ aina ya Yutong lililokuwa likitokea Dar es Salaam baada ya abiria
wote kushuka ndipo alipolikurupua kwa nguvu na kumshinda hatimaye
kuparamia ukuta.
Abiria aliyefariki alikuwa
safarini kuelekea masomoni mkoani Tabora na wakati gari likiparamia
ukuta wa mgahawa huo alikuwa akipata chakula cha jioni
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Jeshi la Polisi imesema licha ya mmoja huyo kupoteza maisha, lakini watano wamejeruhiwa.
Aidha kondakta wa basi hilo
alitoroka na kwenda kusikojulikana na juhudi za Jeshi la Polis kumtafuta
zinaendelea na hadi sasa dereva wa basi hilo anashikiliwa na Polisi kwa
mahojiano zaidi.
Kwa
upande wake Noah Mwakatumbula Mwenyekiti wa Kituo cha Mabasi mkoani
Mbeya yaendayo mikoani amewataka madereva waliopewa dhamana ya kuendesha
vyombo hivyo na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waache mara
moja tabia ya kuacha funguo za vyombo vyao vya usafiri. Habari hii kwa hisani ya MbeyaYetu.Blog
No comments:
Post a Comment
Tafadhari Maoni Yenye Matusi Hayatakuwa Publish Tutoe Maoni Bila Kuumiza Wala Kujeruhi Hisia Za Mtu.....@(Sponsored By Lukaza Blog)